SAJUKI, MWACHENI MUNGU AITWE MUNGU

SAJUKI, MWACHENI MUNGU AITWE MUNGU HEBU mwacheni Mungu aitwe Mungu! Hatimaye habari njema kutoka katika Hospitali ya Saifee iliyopo jijini Mumbai, India anakotibiwa staa wa filamu za Kibongo, Sadick Juma Kilowoko ‘Sajuki’ zinatia faraja kwa Watanzania, Ijumaa Wikienda linakupa stori ‘exclusive’ kutoka nchini humo.

Habari hizo njema zinaeleza kuwa Sajuki aliyeambatana na mkewe, Wastara Juma na kaka yake, hatimaye ameweza kunyanyuka kitandani na kuongea tofauti na siku aliyoondoka Bongo na mwanzoni alipofikishwa hospitalini hapo.
Akizungumza na Ijumaa Wikienda, mwishoni mwa wiki iliyopita kwa njia ya simu, Wastara alisema Sajuki alikuwa amepata nafuu na hali siyo mbaya kwani alikuwa na uwezo wa kuzungumza hivyo akampa simu ili azungumzie afya yake yeye mwenyewe jinsi anavyojisikia.


Sajuki alipopewa simu alianza kwa kuwashukuru wale wote wanaomuombea dua na kujitolea kwa hali na mali ili kuokoa uhai wake.
“Namshukuru sana Mungu naendelea vizuri. Nilichukuliwa vipimo na nikabainika kuwa na uvimbe mwingi sehemu mbalimbali tumboni.
“Madaktari walibaini kuwepo kwa uchafu kwenye mapafu. Mwanzoni waligundua nina tatizo la kupumua na kukaukiwa damu.
“Wamelishughulikia hilo kwanza na hapa nilipo nimezungukwa na madawa, kwa kweli najisikia nafuu,” alisema Sajuki kwa sauti ya kukwaruza.


Sajuki alisema alipokelewa vizuri lakini kabla ya kuanza matibabu ya uvimbe tumboni, madaktari walilazimika kumtibu kwanza tatizo la damu na pumzi hivyo matibabu ya kilichompeleka hospitalini hapo (uvimbe) yakawekwa pembeni.

Kwa upande wake, Wastara alisema kuwa Sajuki alipaswa kupatiwa matibabu kwa wiki mbili ndipo warejee nyumbani lakini kwa hali halisi inaonekana watakaa zaidi kwani tayari wiki mbili zimekatika.

Wastara alisema kuwa baada ya kumalizika kwa tatizo la pumzi na kupungukiwa damu, madaktari wameanza vipimo vya tatizo la uvimbe na kusisitiza kuwa uzi ni uleule wa kumwombea mumewe ili arejee katika siha njema.

Sajuki alianza kusumbuliwa na uvimbe mwaka jana ulioanzia mkononi na baadaye ndani ya mwili kwenye ini na sasa madaktari wanasema siyo kwenye ini tu bali na sehemu nyingine tofauti za tumboni.

Kama alivyosema Wastara, tuzidi kumuombea dua Sajuki ili arejee katika ulingo wa filamu aendelee kutuelimisha na kutuburudisha tunapokuwa majumbani mwetu.

No comments:

Post a Comment