Meneja wa Manchester City, Roberto Mancini, ameonyesha hana uhakika
ikiwa ataendelea kumchezesha Mario Balotelli katika kikosi chake siku
zijazo, baada ya mchezaji huyo kuonyeshwa kadi nyekundu katika mechi yao
dhidi ya Arsenal, na ambayo City walifungwa goli 1-0.
Balotelli, kutoka Italia, aliondolewa baada ya kufanya makosa mawili
makubwa, na kuiacha City katika hali mbaya, ikiwa imeachwa kwa pointi 8
na Manchester United, na ambayo inaongoza ligi kuu ya Premier.
Balotelli pia alimchezea vibaya Alex Song, tukio ambalo mwamuzi
hakuliona, na chama cha soka cha FA kitachunguza madai kuhusiana na
kitendo hicho.
Mancini alipoulizwa kama kuna uwezekano wa kumuuza mshambulizi Balotelli, alisema: “Inawezekana”.
Alikubali kwamba Balotelli,l ambaye amefunga magoli 17 alipoichezea
Man City katika mechi 31 msimu huu, huenda asicheze tena msimu huu.
“Ninampenda kama mtu na mchezaji,” aliongezea Mancini, ambaye
alimsajili Balotelli kutoka kwa Inter Milan ya Italia kwa pauni milioni
24 mwezi Agosti mwaka 2010.
“Ni mtu mzuri na ni mchezaji mzuri sana, lakini ninamsikitikia kadri anavyoendelea kupoteza kipawa chake na ubora wa soka yake.
“Sina lolote la kuelezea kuhusu tabia zake.
“Natumaini yeye mwenyewe atatambua kwamba yumo katika hali mbaya
katika kuangazia hatma yake na ataweza kubadilisha mwenendo wake. Lakini
nadhani hatacheza katika mechi sita zijazo.
“Ninahitaji kuwa na uhakika wakati wote kuwa na wachezaji 11 uwanjani katika mechi, na kumtumia Mario ni kubahatisha.”
Balotelli alitimuliwa baada ya kumchezea vibaya mara mbili Bacary
Sagna, muda mfupi kufuatia Mikel Arteta kuifungia Arsenal bao la ushindi
katika dakika ya 87 katika mechi.
Hii ni mara ya pili msimu huu kwa Balotelli kutimuliwa katika mechi.
Mancini aliongezea: “Ni kijana mdogo na anaweza kuwa mwanangu, na ukiwa kijana, unaweza kufanya makosa”.
No comments:
Post a Comment